Thursday 4 September 2014

WILLIAM LUKUVI AZOMEWA MBELE YA RAIS JK





Dodoma. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi amejikuta katika wakati mgumu mbele ya Rais Jakaya Kikwete baada ya kuzomewa hadi kukatisha hotuba yake akipingwa na wananchi pamoja na madiwani wa CCM wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma alipokuwa akitetea kuwapo kwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA).
Lukuvi alikumbana na mkasa huo wakati akijibu hoja za Mbunge wa Dodoma Mjini (CCM), David Malole ambaye alitaka CDA ivunjwe akiituhumu kuwavunjia wananchi nyumba bila kuwatafutia mahali pa kuishi.
Kuzomewa
Baada Malole kutoa madai hayo, Lukuvi ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya CDA alilazimika kupanda jukwaani ili asawazishe kauli za mbunge huyo, jambo ambalo liliibua zogo na wananchi kuzomea.
Zomeazomea dhidi ya Lukuvi ilitawala katika kipindi chote alichokuwa jukwaani huku viongozi wa chama wakihaha kuwazuia wanachama na madiwani wa CCM wasizomee bila mafanikio.
Hali iliendelea kuwa mbaya kwa Lukuvi pale aliposema, “Mimi ni mdau mkubwa wa CDA na ni kati ya watu ambao walishiriki kupeleka maendeleo katika Mji wa Dodoma.”
Kauli hiyo ilisababisha madiwani pamoja na wananchi kuanza upya kumzomea huku wakimtaka ashuke jukwaani kwa madai kuwa hana cha kuwaeleza hadi wamwelewe.
Hali hiyo iliambatana na nyimbo zilizoanzishwa na madiwani, “CCM.. shuka chini, CCM shuka chini” hali iliyomfanya Lukuvi kushuka jukwaani.
Baadaye Rais Kikwete akizungumza na wakazi hao, alitoa siku saba kwa viongozi wa mkoa kwa kushirikiana na mbunge kukaa na kutatua mgogoro huo na aliahidi kukutana nao Septemba 8, mwaka huu.
Alisema migogoro haiwezi kutatuliwa katika mikutano ya hadhara, bali vikao vya kazi. Aliwataka kukutana kuangalia ni jinsi gani watamaliza mgogoro huo bila kuwa na fujo wala lawama.

No comments:

Post a Comment